Bavicha yathibitisha kuwatimua vigogo - Arusha Forum
Headlines News :
Home » » Bavicha yathibitisha kuwatimua vigogo

Bavicha yathibitisha kuwatimua vigogo

Written By Sema Naye - Naipenda Tanzania on Tuesday, January 8, 2013 | 11:40 AM

Na Mwandishi wetu
8th January 2013
Mwenyekiti wa Bavicha, John Heche

Kamati ya Utendaji ya Baraza la Vijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Bavicha), limethibitisha kuwatimua uongozi na kisha kuwavua uanachama wajumbe watatu wa Baraza hilo akiwamo Makamu Mwenyekiti wake Taifa, Juliana Shoza.

Mwenyekiti wa Bavicha, John Heche, alisema kamati ilikutana Januari 5, mwaka huu na kujadili mambo matatu ambayo ni kuporomoka kwa elimu nchini, Bavicha itakavyoshiriki katika maandalizi ya utekelezaji wa maazimio ya Kamati Kuu ya Chadema.

Heche alisema kikao hicho pia kilijadili tuhuma za usaliti na njama za kukivuruga chama, kuwatukana viongozi wakuu wa chama na kuvuruga wanachama wa Chadema na Baraza Kuu.

Alisema Kamati ilipewa mwezi mmoja kukamilisha kazi hiyo na watuhumiwa wakuu walikuwa ni Juliana Shonza (Makamu Mwenyekiti), Habibu Mchange, Mtela Mwampamba, Gwakisa Mwakasendo, Joseph Kasambala, wanachama wa  Bavicha na Chadema.

Alisema baada ya kamati iliyoundwa kuwahoji baadhi ya watuhumiwa na wanachama wengine, ilibaini kwamba wapo wanachama wa Bavicha walioshiriki kwa namna moja au nyingine katika tuhuma hizo ambao ni  Ben Saanane, Exaud Mamuya, lakini kamati ilishindwa kumpata Mamuya kwa sababu hakukuwa na mawasiliano ya kutosha.

Heche alisema Shoza anatuhumiwa kwa makosa mbalimbali yakiwamo kupanga njama na kufanya usaliti dhidi ya Baraza, Chama na vijana wenzake wapenda mabadiliko, kufanya vikao vya siri kwa manufaa ya CCM, kuchonganisha wanachama ma kutukana chama na viongozi wakuu.

Tuhuma zingine ni pamoja na kuwakusanya wanafunzi wa vyuo vikuu mbalimbali waliosimamishwa masomo au kufukuzwa vyuoni kwa kutimiza wajibu wao wa kudai haki zao za msingi na uwajibikaji wa serikali na ambao ni wanachama wa Chasso.

Heche alisema Shonza pia alishiriki kuanzisha chama Chama cha Ukombozi wa Umma (Chauma), kushiriki katika makundi yaitwayo Masalia na PM7-pindua Mbowe (Freeman) ambayo yote yalikuwa na lengo la kuvuruga, kukosanisha na kutukana viongozi wa chama, na kuvunja kipengele cha 10.1(i),(viii)(ix) na ibara ya 10.2(iv).
Tuhuma zingine ni kuhusika katika kuanzisha, kujihusisha na kuratibu kundi la vijana waliokuwa wakizunguka mikoani na kushawishi viongozi wa vijana kutoa matamko kwa kutumia jina la Chadema kufanya kazi na majukumu ya CCM ya kukichafua chama, kugombanisha wanachama na kumtukana Katibu Mkuu (Dk. Wilbrod Slaa) kwa kutumia propaganda za CCM.

Heche alisema kutokana na tuhuma hizo, kamati ndogo ilimuita Shonza ili kumhoji, lakini aligoma kwa madai kuwa haitambui kamati hiyo na wala hajui kuwa kuna mgogoro, jambo ambalo liliwashangaza wengi .

Alisema Shonza amepoteza sifa na uhalali wa kuwa mwanachama wa Chadema kwa kukiuka ibara ya 5.3.4 na ibara ya 10.1(ix) ya katiba ya Chadema na hivyo imeamua kumuondoa katika nafasi yake ya makamu mwenyekiti na kumfuta uwanachama wake.

Waliofukuzwa wengine kwa makosa mbalimbali ni pamoja na  Abibu Mchange,Mtela Mwampamba.

Heche alisema Kamati pia imewaonya wanachama wawili na kuwapa adhabu kali ya uangalizi wa miezi 12 ambao ni Ben Saanane na Gwakisa Mwakasendo kwa kuwa walikiri kuhusika na makosa na kuomba msamaha mbele ya kamati.

Viongozi hao waliotimuliwa watazungumza na waandishi wa habari leo.
 
CHANZO: NIPASHE
Share this article :

0 comments:

Speak up your mind

Tell us what you're thinking... !

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. Arusha Forum - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website Published by Mas Template
Proudly powered by Blogger